Loading...

WATU ZAIDI YA MILIONI 40 WAHAMA DUNIANI

Loading...
KUNA wahamaji milioni 41 Afrika ambapo karibu nusu ni wanawake ambao huenda kufanya kazi za ndani kwenye nyumba za wakazi wa nchi wanazohamia kwa lengo la kutafuta kipato.

Akizungumza jana katika uzinduzi wa Ripoti ya Maendeleo ya Kiuchumi Barani Afrika ya mwaka 2018, Mkuu wa Masuala ya Afrika wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Masuala ya Biashara na Maendeleo (UNCTAD), Junior Roi Davis, alisema:

Ajira za wanawake haziangalii uwezo wao kitaaluma bali jinsia, hivyo jinsia hiyo ambayo ni asilimia 47 ya wahamaji hupewa kazi za ndani pekee.

Alisema utafiti huo umebaini kuwa watu milioni 41 walihesabiwa kama wahamaji, ikiwa ni watu milioni 19 waliohama nchi moja kwenda nyingine Afrika, milioni 17 waliokwenda nje ya Afrika na milioni 5.5 walitoka sehemu nyingine kuja Afrika.

“Ushiriki wa wanawake unachangia kuinua uchumi licha ya kuwapo kwa changamoto mbalimbali, tunachoshauri ni kuwapo kwa taratibu za kusaidia kuwepo kwa haki ya ajira kwa wahamiaji wanawake na siyo kuishia kufanyakazi za ndani pekee,” alisema.

“Kuna waliotoka nchi za Ulaya, China na India kuja Afrika kama wahamiaji ambao waliona fursa mbalimbali za kiuchumi… uhamaji hauko kwa watu wanaotoka Afrika kwenda nchi za Magharibi pekee bali wapo wanaotoka nchi zilizoendelea kuja Afrika.”

Kwa mujibu wa Davis, ripoti hiyo imelenga kutoa ushauri na mwongozo wa sera na taratibu au mienendo mbalimbali na hatua za kuboresha uchumi kwa nchi za Afrika, kwa kuwaangalia wahamaji kama fursa muhimu ya kushirikiana nao kwenye uwekezaji na biashara badala ya kuwaona wanachukua ajira na fursa zao.

Aidha, alisema nchi za Ivory Cost, Rwanda, na Afrika Kusini zimeongoza kupokea wahamiaji wenye taaluma mbalimbali na wamesaidia katika maendeleo ya kiuchumi, ikiwamo kuwekeza katika miradi iliyoajiri maelfu ya wazawa.

“Uhamaji siyo kwamba ni tishio pekee bali husaidia wengi kutoka kwenye umaskini kwa kuwa sekta zinazonufaika moja kwa moja ni kilimo, huduma na migodi, ikiwa ni pamoja na kuinua hali ya kufanya biashara,” alifafanua Davis na kueleza zaidi:

“Asilimia 85 ya fedha za wahamaji zilitumwa nyumbani kwao, mwaka 2014 hadi 2016 fedha zilizotoka nje ya Bara la Afrika kwa wahamaji wanaoishi nchi zilizoendelea ilikuwa ni Sh. bilioni 64.9, asilimia 51 zilipita kwenye akaunti za mtu mmoja mmoja ambaye ni mwanafamilia.

“Changamoto kubwa ni gharama kubwa za kuhamisha fedha jambo ambalo limesababisha wengi waache kutuma fedha kwa ajili ya uwekezaji nyumbani.”

Davis alisema utafiti huo umebaini kuwa fedha zote zilizotumwa ziliingia kwenye miradi ya uwekezaji, ambayo ilisaidia kuinua uchumi na kufungua fursa za ajira kwa watu wa nchi husika.

Ripoti hiyo imetoa mapendekezo ya kuiga mfano wa Rwanda na Morocco ambazo zimewachukua wahamaji kama fursa ya kuendeleza nchi zao, na mara kadhaa wamefanya vikao na waajiri kuangalia namna ya kutatua changamoto ya ukosefu wa ajira ambayo ndiyo huwakimbiza vijana wengi kwenda nchi zilizoendelea.

“Tunashauri nchi za Afrika kuangalia suala la usawa wa kijinsia katika kushughulikia wahamiaji hasa wanawake, kuwepo sera ya kuwasaidia na siyo kuwaangalia kama kikwazo cha fursa za biashara, uwekezaji na maendeleo.”

Aidha, alisema ni vyema nchi za Afrika kupitia Jumuiya zao wakatafakari wimbi la vijana wanaomaliza vyuo vikuu na kukosa ajira, kwa kuangalia namna ya kushirikiana na wahamaji wenye ujuzi wa kuanzisha shughuli za kibiashara ambao zitaajiri watu na badala ya kuwaona kama wahamiaji pekee.

Aidha, ripoti hiyo imebaini kuwa sababu kubwa ya watu kuzihama nchi zao ni suala la kiuchumi ambalo lazima lipatiwe ufumbuzi kwa kutafuta visababishi na kuvifanyia kazi kupitia jumuiya.
Na Paskali Joseph.



Una maoni? Una habari ambayo ungependa tuichapishe? Tuma ujumbe kwa mhariri mkuu:dundiikaonline@gmail.com au sms-whatsapp: +255765112259
WATU ZAIDI YA MILIONI 40 WAHAMA DUNIANI WATU ZAIDI YA MILIONI 40 WAHAMA DUNIANI Reviewed by By News Reporter on 6/02/2018 07:57:00 AM Rating: 5

Hakuna maoni:

Loading...
Inaendeshwa na Blogger.