Loading...

WANAUME NCHI NZIMA KUPIMWA VIRUSI VYA UKIMWI

Loading...
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema mwezi ujao, atazindua kampeni maalum ya upimaji wa virusi vya Ukimwi (VVU) ambayo inalenga kuwahamasisha wanaume nchi nzima kupima afya zao na kutambua hali zao.

“Serikali tumeandaa kampeni maalum ya kuhamasisha upimaji wa VVU na kuanza matumizi ya dawa za kufubaza VVU mara moja, hasa kwa wanaume. Kampeni hii itazinduliwa rasmi na mimi mwenyewe jijini Dodoma 19 Juni 10,” alisema jana.

Alisema hayo jijini Dar es Salaam, wakati akizindua maadhimisho ya miaka 15 tangu kuanzishwa kwa Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kupambana na Kudhibiti Maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (PEPFAR).

“Takwimu zinaonyesha watu ambao wako tayari kupima kwa hiari yao siku zote ni wanawake. Kinababa wakiambiwa hutoa sababu mara hiki, mara kile. Nitoe wito kwa wanaume wote, tubadilike! Ni vema tushiriki kampeni ya wanaume kujitambua na kupima ili tujue hali zetu,” alisema.

Amewataka wadau wa masuala ya Ukimwi washiriki kikamilifu katika kampeni hiyo baada ya uzinduzi na pia kuwataka wakuu wa mikoa yote wasimamie kampeni hizo muhimu katika mikoa yao hadi ngazi za vijiji.

Waziri Mkuu alisema ujio wa PEPFAR umeleta mafanikio makubwa katika vita dhidi ya Ukimwi na kupitia shughuli zake, elimu ya kinga na ufahamu kuhusu ugonjwa huo ilitolewa kwa watu wa rika na makundi mbalimbali ya jamii.

Hata hivyo, Waziri Mkuu alisema Tanzania inaendelea kukabiliwa na changamoto kadhaa zikiwamo ukubwa wa viwango vya maambukizi na kuongezeka kwa idadi ya watu wanaoambukizwa VVU katika baadhi ya mikoa nchini.

Kwa mujibu wa Majaliwa, kuna mikoa 14 ambayo kiwango cha maambukizi kiko juu ya wastani wa kitaifa wa asilimia 4.7 na kuitaja ni Njombe asilimia 11.4, Iringa (11.3), Mbeya (9.3), Mwanza (7.2), Kagera ( 6.5) na Katavi (5.9).

Mingine ni Shinyanga (asilimia 5.9), Songwe (5.8) Ruvuma (5.6) Pwani (5.5) Tabora (5.1) pamoja na Tanga, Dodoma na Geita ambayo yote ina asilimia 5.0 ya maambukizi.

Waziri Mkuu aliitaja mikoa mingine sita ambayo ina ongezeko kubwa la watu wanaoishi na VVU ni Iringa (asilimia 11.3), Mwanza (7.2), Kagera (6.5), Tanga (5.0), Dodoma (5.0) na Manyara (2.3).

Alifafanua takwimu hizo zinaonyesha kuwa nguvu na jitihada zaidi zinahitajika katika kuzuia maambukizi mapya ya VVU kwa kuweka utaratibu thabiti na endelevu wa kutoa elimu na hamasa ya kutumia huduma zilizopo za kupambana na UKIMWI nchini.

“Kwa hiyo, programu za kinga zinapaswa kuwa endelevu kwenye mikoa yote nchini, hususan mikoa yenye kiwango cha juu cha maambukizi. Pia huduma za ARV ziendelee kupewa kipaumbele katika mipango yetu,” alisisitiza.

Akimkaribisha Waziri Mkuu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema Tanzania kwa sasa ina watu karibu milioni moja ambao wako kwenye matibabu ya kufubaza VVU.

“Kutokana na mpango wa PEPFAR, Tanzania imeshapokea Sh. trilioni 10 tangu mfuko huu uanzishwe mwaka 2003 na matumizi ya dawa za kufubaza VVU yamesaidia kupunguza idadi ya vifo vitokanavyo na Ukimwi kwa asilimia 70, yaani kutoka vifo 110,000 mwaka 2003 hadi kufikia 33,000 mwaka 2016,” alisema.

Alisema kutokana na matumizi ya dawa hizo, maambukizi mapya kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto nayo pia yamepungua kutoka asilimia 12 na kufikia 4.9.

Kaimu Balozi wa Marekani nchini, Inmi Patterson, alisema kati ya sasa na Septemba 2019, PEPFAR inatarajia kutumia dola za Marekani milioni 512 (zaidi ya Sh. trilioni moja) katika kuboresha huduma za kuzuia maambukizi ya VVU, upimaji na matibabu nchini.

Alisema wanapoendelea na utekelezaji wa kazi za mfuko huo na maadhimisho ya miaka 15 ya PEPFAR, kampeni yao itaendelea kwa mwaka wote wa 2018 na imelenga kupunguza unyanyapaa na tabia ya kuwatenga watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi.

“Kampeni ya PEPFAR15 inalenga kupunguza unyanyapaa, kuongeza upatikanaji na matumizi ya huduma zitolewazo za kukabiliana na VVU. Kila mtu atakayepimwa na kugundulika kuwa ana maambukizi ya VVU, ataanzishiwa matibabu mara moja,” alisema na kuongeza:

“Tutafanya kazi na watu wanaoishi na VVU nchini kote ili kusimulia habari nzuri za watu wanaoishi na VVU ambao waliwahi kuwa dhaifu ama wagonjwa, lakini sasa wana nguvu na afya; habari za akinamama wanaoishi na VVU na wanapata matibabu ili kuwalinda watoto wao.”

Na Geofrey Okechi.




Una maoni? Una habari ambayo ungependa tuichapishe? Tuma ujumbe kwa mhariri mkuu:dundiikaonline@gmail.com au sms-whatsapp: +255765112259
WANAUME NCHI NZIMA KUPIMWA VIRUSI VYA UKIMWI WANAUME NCHI NZIMA KUPIMWA VIRUSI VYA UKIMWI Reviewed by By News Reporter on 6/01/2018 10:11:00 AM Rating: 5

Hakuna maoni:

Loading...
Inaendeshwa na Blogger.